Thursday, March 26, 2009

TUTAANZAJE UPYA BILA FIKRA MPYA?

Mijadala ni mwanzo wa kuibuka kwa fikra mpya na changamoto kuelekea maendeleo ya kijamii. Pasipo mijadala mawazo yamefungwa, yanabaki vichwani tu. Mijadala isiyokamilishwa na matendo ya kuyatekeleza ni mijadala iliyokufa.Haitufai.

Ni dhahiri yako mengi yasiyo sawa, ndani ya jamii na yanayotuzunguka, ndani ya daladala, radioni kunasikika hotel ya Paradise imeungua, iko Bagamoyo.Bagamoyo gari ya zimamoto hakuna, jamaa anaongea kwa sauti kuuuubwa, anauliza “gari moja ya zima moto shilingi ngapi hata kuishinda wilaya kama Bagamoyo kulimiliki”? Hotel imeungua. Imeteketea. Hatuoni. Hatusikii. Hatubadiliki.

Hapa ndipo watu wanajiuliza,” ni nani aliyeturoga?”, tuangalie kwa uchache baadhi ya mambo.

Elimu yetu, ni kwa vipi inatusaidia kutatua matatizo yetu?, ni kwa vipi inaikabili hali ya umaskini inayotuzunguka?, ni kwa vipi imejipanga kukabilianana mahitaji halisi ya jamii yetu?, ni kwa vipi inapunguza pengo la kiteknolojia lililopo kati yetu na mataifa yaliyoendelea litufanyalo tuendelee kuwaabudu ‘wazungu’ kuwa wenye akili sana kana kwamba waafrika tumezaliwa tukiwa ni “vilaza”?, Inawaandaaje watu wetu kuwa wavumbuzi siku zijazo?, Inawaandaaje watu wetu kulima kilimo cha kisasa?, Inawaandaje watu wetu kujikinga na maradhi kama malaria na kipindupindu?,
Ni kwa vipi imejipanga kukabiliana na mahitaji halisi ya jamii yetu?, tunaambiwa waalimu tulionao ni wachache, nini kinafanyika kuondoa tatizo hili?, na kama kuna linalofanyika ni kwa ubora gani?. Kuna wakati ilikuwa fahari kusoma shule za Serikali kuanzia shule ya msingi hadi sekondari.Hali si hivyo sasa. Aanyebisha na ajitokeze!. Watu wenye uwezo wa kifedha hawapeleki wana wao kwenye shule hizo.Viongozi wetu hawapeleki wana wao shule hizo. Zimekuwa shule za kina Kayumba!, Wenye uwezo wanasomesha wana wao shule za seminary, shule za mtakatifu fulani na fulani, wakilamaliza wanawapeleka vyuo vya nje.Wanatudanganya kwa kuonyesha uzalendo wao kwenye kuchangia mabati ya shule na madawati. Mbona watoto wao hawasomi huko?, Kwa nini tusiwaambie wabunge na madiwani wetu kuwa kama watoto wenu hawasomi shule zetu na nyinyi si wenzetu?, kama watoto wao wangesoma shule zetu, zingekosa walimu?, zingekosa madawati?, wasingezijali?
Turudi kwa walimu, nani asiyejua kuwa huu ni uchaguzi wa mwisho wa wanafunzi wetu wanapokosa vyuo vingine vyooote!, hii imepelekea wanafunzi wanaopata daraja la nne ndio hufikiria kuomba kudahiriwa kwenye vyuo vya ualimu.Bado tunadhani tuna elimu bora?
Mbali na hapo waalimu hao wachache na baadhi wenye ubora mdogo wanahama taaluma yao muda mfupi baada ya kukabiliana na ugumu wa mazingira ya kazi wakiwa ndani ya ajira zao

Uchumi wetu, madini tuliyonayo kwa uchache tukitaja dhahabu, almasi na tanzanite bado hayajatuletea tija ya kutosha. Mwalimu Nyerere aliwahi kutuasa kuwa tuyaache madini yetu hadi pale tutakapoweza kuyachimba wenyewe kwa kutumia wataalamu wetu. Wajanja wakaja na pipi wakatuzidi akili tukawaachia, eti wawekezaji.Wizi mtupu!.Tunaambiwa wanatuachia 3% tu ya mapato, na sisi ndio wenye mali. Si wizi huo?. Geita,Tulawaka, Bulyankulu, Buzwagi, Kahama, North Mara iko siku tutashuhudia mashimo mareeeeeeeefu, sijui tutawajibu nini wana wa wanetu pale watakapotuuliza kilichotoka kwenye mashimo hayo tulikiuza wapi, shilingi ngapi na tulitumiaje kilichopatikana?. Bila shaka uwekezaji ( niuite wizi) huu uliofanyika katika madini yetu mithili ya huo duniani haupo!.Tunaambiwa mmmoja wa mikataba hiyo ulisainiwa Uingereza na waziri husika.Inasemekana shughuli hiyo ilifanyika hotelini. Nani aliyeturoga watized sie?

Samaki, ndio tumeibiwa mpaka basi. Majuzi kuna meli imekamatwa na tani 200 za samaki, kilo moja ni dola 20, tani 200 ni kilo 200,000, hivyo gharama ya wizi ule uliozuiwa ni 4000,000$, kwa kiwango cha kubadilisha dola cha sasa 1300/=, tungepoteza billioni 5.2 fedha za kitanzania. Wajinga ndo waliwao, duh!, wale wachina, wavietinam,ufilipini, indonesia na wakenya watatu, arobaini yao ilikuwa imefika, kesi iko mahakamani sasa. Kazi kwao.Kabla ya hizo arobaini zao, anzia moja, mbili, tatu,……… hadi arobaini, ni shilingi ngapi zilizoibiwa?, kama ndio ilikuwa kamchezo kao jamaa, tuwapigie hesabu 40-1=39; 39 zidisha kwa bilioni 5.2 ni sawa na bilioni 202.8/=.Wizi mtupu!. Tones na tones za samaki wetu wa baharini na maziwani zinaenda Ulaya.Uwiano wa mapato na kinachochukuliwa ( kinachoibwa) ni mdogo saana!. Maziwa na bahari zetu nazo ni shamba la bibi?, kila mtu anavuna na kula!, bibi hana noma!,eti wacha wajukuu wale!, tuseme nini basi kama si kulogwa ni nini?. Nani wa kutukomboa na giza hili?.Hakika bado tungali gizani hata katika mwanga huu!
Wako wapi wenye taaluma ya viumbe hawa wa majini?, Je tuna mabaharia wa kutosha katika shughuli hizi za majini?, Ulinzi wa majini uko bora kwa kiwango kinachostahili?, walikovua samaki wetu hao wezi, je sisi tuna meli gani tunazozitumia kuvua huko?,Au kuvua hatuvui samaki wetu lakini kuibiwa hatutaki?

Maadili yetu, hapa napo panazingua!. Sielewi ni nani mlinzi wa maadili yetu kama si sisi wanajamii wenyewe?, nani anayekemea mmong’onyoko wa maadili unakwenda kwa spidi ya swala katika jamii yetu?, Waangalie dada zetu, ni uchizi kama si uwendawazimu, hakuna nguo za siri tena kwani leo hii ni kawaida kuwaona mabinti wamevaa chupi zikiwa juu ya suruali zao za kubana, wanazionyesha za nini?, wanamuonyesha nani?,ili iweje?. Nguo fupi na viblauzi vya kuishia juu ya kitovu, eti fashion.Sijui. Ila nionavyo tuendako hakuna maelezo ya kutosha kuelezea yatakayojiri kwa wana na wana wa wana wa taifa hili! Mashuleni na vyuoni ndipo yalipotamalaki mambo hayo wanayoita ‘kwenda na wakati’!

Naungana na wanaosema tunahitaji mijadala ya kitaifa katika kutatua matatizo yanayotuzunguka.

Tufanye hivyo!.

Tuanze sasa!

Mijadala hujenga fikra!

Mungu ibariki Tanzania!

Wednesday, March 25, 2009

BILLY GRAHAM AND US PRESIDENTS!

David Frost ndiye muandishi, ni habari inayoeleza nyuma miaka 30 Mazungumzo yao na Billy Graham katika kitabu kiitwacho “Personal thoughts of a public man”

Billy Graham ni mhubiri wa kimataifa, anafahamu siasa za Marekani na amekuwa rafiki wa karibu wa karibu kila raisi wa taifa hilo kubwa kama vile,Harry Truman, Eisenhower, Lyndon Johnson ,John Kennedy, Richard Nixon na Bill Clinton.

Ukurasa wa 95
President Bill Clinton, May 6, 1996 alinukuliwa akisema:

‘I hardly ever go to a place, as Presiident, that Billy Graham has not been there before me preaching. And I feel like a poor substitute, because a lot of the time what I’m trying to do is to get people to lay down the hatred of the heart and reach down into their spirit and treat people who are different from themselves with the same respect that all God’s children are entitled to…………………..
I thank Billy and Ruth Graham for the ministry of their lives’

Ukurasa wa 97;

David Frost, mwandishi wa kitabu hichio: anasema ‘No preacher in the history of this country has had so much access to many presidents as Billy Graham’.



Hapana shaka kuwa alikuwa mshauri wa kisiasa wa wakuu hawa wa Marekani, ushauri uliobeba ukweli na sera zenye kubeba haki na demokrasia.

Marekani ya leo inayoongozwa na Rais Obama, mweusi, ni dhahiri kuwa ni mwendelezo wa harakati fulani za hadharani kama za kina Martin Luther na kina Billy Graham.`

Hapa tunajifunza kuwa viongozi waongozao roho zetu wana nafasi kubwa ku ‘influence’ siasa zetu, hapa Afrika na hasa Tanzania katika kujenga jamii bora zaidi,yenye hofu ya Mungu na kusimamia haki. Na si kuendekeza ufisadi unaolimaliza bara la Afrika. Mfano mzuri wa mapambano haya na harakati za kuipigania haki ni Askofu Desmon Tutu wa Afrika ya kusini. Ambaye wakati Mandela akiwa gerezania alionekana hadharani akiongoza maandamano ya kuidai haki ya usawa ndani ya nchi yao na kuna wakati aliwakemea watawala wa Afrika a kusini, wabaguzi,, kwa sauti kuuuubwa “ Release our leaders”, “Release our leaders”, “Release our leaders”. Bado watanzania tumo katika kifungo cha umasikini, maradhi, ujinga, ufisadi. Nani wapigao kelele mithili ya Desmond Tutu akiwataka watawala wetu na wakoloni wetu wa kale kutuacha huru.


Wako wapi kina Billy Graham wetu Tanzania!