Tuesday, December 25, 2007

Wednesday, October 24, 2007

GAZETI JIPYA RAIA MWEMA!

Moja ya magazeti ambayo nilitokea kuyapenda kwa muda mrefu sana ni gazeti la Rai.Hii ilitokana na umakini na ujasiri wa waandishi wa gazeti hili.Ninaamini kabisa kuwa magazeti yana sehemu kubwa katika kujenga fikra zetu, kutufundisha, kutuelimisha, kutuburudisha na kutuonyesha uozo, au tuuite ufisadi, ndani ya jamii yetu na hata namna ya kupambana na uozo huo. Magazeti yakiandika habari za kweli na kwa uwazi yataweza kuisaidia jamii yetu kusonga mbele kifikra na kimaendeleo.

Nakiri kwa kusema kuwa hamu ya kulisoma gazeti la Rai imenitoka,siku hizi nalinunua kwa mazoea tu, umakini na uandishi wa gazeti hili sio ule wa walipokuwa wakiandika akina Jenerali Ulimwengu na Maggid Mjengwa.Nadhani sasa gazeti hili jipya la “Raia Mwema” litaziba pengo lililoanza kujitokez andani ya Rai, sijui gazeti la Rai limekumbwa na nini.Sielewi!

Muda mfupi nimeisoma habari ya kuanzishwa kwa gazeti hili, na wiki ijayo inatoa toleo la kwanza, miongoni mwa waandishi ni Jenarali Ulimwengu, Prof Issa Shivji,Maggid Mjengwa, Mihangwa na Padri Pivatus Karugendo.Kama unawafahamu waandishi hawa basi usikose kusoma makala zao!.Utaniambia mwenyewe!

Sina shaka na hawa waandishi kuwa kuwa wamekubuhu katika taaluma ya uandishi wa habari, watakuwa na ujasiri wa uandika yale ambayo wengine wameogopa, watashiriki katika mchakato wa kuisafisha jamii yetu inayoendelea kuchafuliwa na ufisadi, utandawizi na mmong’onyoko wa maadili.

Kila la kheri gazeti la “RAIA MWEMA” ninaahidi kukunua kila utokapo!

Sunday, October 21, 2007

WATU WAOVU WAMEMUUA LUCKY DUBE!

Ni mchana wa ijumaa niko sehemu napata msosi wa mchana, pembeni jamaa anaongea na mwenzake, Lucky Dube amefariki, nayasikia maongezi yale, kwa kuwa sikuwa mbali na meza yao.Nashangaa!.Namuuliza mmoja wao , ananiambia ni kweli jamaa wamemuua Lucky Dube.Jioni siku hiyo hiyo ya ijumaa nasikiliza Voice of America, nasikia wanatangaza kuwa Lucky Dube ameuwawa.

Nikiwa njiani nakutana na ajali daladala,DCM, imeuvaa mti, mtu mmoja amefariki, mwili wake ukiwa bado umelala barabarani!
Maisha ni safari yenye mwisho,hakuna ajuaye mwisho huu unafika lini!,Lucky Dube hakujua kama siku ile angeaga dunia,watu wasio na utu wamemuua, ni watu wenye dhamiri zilizokufa tu, ndio wawezao kufanya kitendo cha kinyama kiasi hicho!

Kijana yule angejua kuwa gari lile lingepata ajali asingalipanda daladala lile!,kifo ni kitu ambacho tumefichwa tusijue kinakuja lini na kwa staili gani!
Anyaway, maisha hayana budi kuendelea!

Ni aina ya uaimbaji wake na ujumbe ndani nyibo zake ndizo zinisukumazo kuandika juu yake.South Afrika na Afrika kwa ujumla imempoteza
mpambanaji dhidi ya ubaguzi wa rangi,mwanamapinduzi na mpigania haki za watu wanyonge Lucky Dube!

He has gone but the messages in his songs will continue to live!

Sunday, October 14, 2007

NYERERE DAY

Ninaikumbuka siku hii ya leo, miaka 8 iliyopita, tarehe 14 october 1999,nikiwa mwaka wa kwanza katika chuo kikuu cha Dar es salaam, kitivo cha uhandisi, nakumbuka tulikwa kwenye kipindi katika karakana ya umeme. Mara tukasikia wimbo wa taifa unapigwa,kila mmoja anaikimbilia radio kisha tunamsikia raisi wa awamu ya tatu,Mkapa anatangaza Mwalimu Nyerere amefariki dunia! Baada ya muda uongozi wa chuo unatoa tangazo la kusimamisha ratiba zote za vipindi.Ilikuwa mshtuko mkubwa.Baada ya siku kadhaa mwili unawasili Tanzania chuo kikapanga utaratibu mzuri wa kuwawezesha wanachuo kwenda kuuaga mwili wa hayati Mwalimu Nyerere,nilikuwa mmoja wa waliofika uwanja wa taifa kuuaga mwili wa Mwalimu, usiku wa manane lakini ilikuwa kama mchana jinsi watu walivyojaa.Umati ule unanifundisha jambo moja 'kuongoza ni kujitoa kwa ajili ya unaowaongoza', Mwalimu aliyatoa maisha yake kwa ajili ya taifa lake, aliishi alichokisema na alisema alichokiishi tofauti na viongozi wetu wa leo!

Tunapoikumbuka siku ya kufariki kwa Mwalimu Nyerere hii leo tujiulize maswali yafuatayo:-

Hivi mwalimu angalikuwepo soo kama la Richmond Development Cooperation lingepita kimizengwe vile na mambo yakaisha kiaina kama yalivyoisha?
Sasa tunaambiwa kuwa mkataba ule ulisainiwa usiku na Tanesco hawajui ni nani aliyeusaini. Inashangaza!

Hivi ule mkataba tata wa madini wa Buzwagi ungepita hivihivi bila kuundiwa tume huru aliyoiomba Mbunge Zitto?
Bila shaka Mwalimu angemwagia sifa Zitto Kabwe hadharani na kuwasuta wabunge wa CCM waliomfukuza bungeni.Bila shaka angesema kuna haja ya waziri Karamagi ajiuzulu!

Hivi ile kashfa ya ufisadi aliyoiibua Dk Slaa, wale waliotajwa angelipuuziwa kama ambavyo wanafunzi wake wamepuuzia? Bila shaka angaliwaita wote Butiama na kuwahoji maswali magumu, na labda angalishauri baadhi yao wajiuzulu!

Hivi Mwalimu angalikuwepo wanafunzi Mlimani wangelipishwa 40% ya ada? Bila shaka angalikemea kwa nguvu zote!

Huyu ndiye Mwalimi ambaye miaka nane sasa bila yeye viongozi wetu wameshindwa kuweka dhamira yao kwa dhati na kwa vitendo kupambana na ufisadi, kwani hata ndani ya chanma alichokiasisi yeye Mwalimu nguvu ya pesa inatumika kupata uongozi!

Miaka minane bila Mwalimu Nyerere ujumbe kwa viongozi wetu ni kuwa, wamuenzi Mwalimu kwa vitendo na si kwa maneno kama wafanyavyo sasa,tumechoshwa na porojo, tumeschoshwa na maneno tunataka vitendo.

Friday, September 28, 2007

HOJA YA KUANZISHWA BLOGU YA WABUNGE NA WANANCHI!

Mara nyingi katika mijadala isiyo rasmi ninayoifanya na watu mbalimbali tunapojadili mambo ya siasa tunakubaliana kuwa tatizo kubwa la siasa ya nchini kwetu ni mfumo mzima unaoendesha siasa.Ni kama vile wananchi hatuna sauti na nguvu ya kuwaaambia wawakilishi wetu bungeni kuwa ni nini tunataka, na wao wakakisimamia kuhakikisha kinafanyika, kwa hali ilivyo sasa ni kama vile wabunge hatujawatuma wametumwa na chama hasa wale wa CCM.Wanasikiliza zaidi chama kuliko wananchi wanaowawakilisha.Mfumo huu haufai na tunaweza kuurekebisha.

Hivi kwa nini kusiwe na blogu, mfano www.wasiliananawabunge.blogspot.com, ambayo itawakutanisha wananchi na wabunge,kabla ya wabunge kwenda Dodoma na wakati wakiwa Dodoma tuwaeleze nini waihoji serikali kwa niaba yetu, na tusiporidhika wakiwa huko huko Dodoma tuwaeleze hatujaridhika na majibu ya Serikali ili wahoji, wahoji na wahoji hadi majibu yapatikane.Vinginevyo tutaendelea kusikia majibu ya porojo ya kila siku wanayojibu mawaziri wetu ,yasiyo na nguvu ya uwajibikaji, majibu kama, serikali iko mbioni kushughulikia swala x,serikali inafuatilia kwa karibu suala y,serikali ina mkakati wa kufanya swala z,serikali imejizatiti kuondoa uasikini ifikapo mwaka f,serikali inafanya kila linalowezekana kuhakikisha kero h inakwisha, majibu haya hayatoshi na yanahitaji maswali mengine zaidi lakini wabunge wetu huridhika nayo.

Wakati umefika sasa wa kuwa na jukwaa la kuwaambia wabunge wetu pale tunapotaka waihoji serikali na tusiporidhishwa na majibu ya serikali.

Blogu hii pia iwe na e mail address na namba za simu za wabunge wote.

Tutaendelea kuyanyoosha yaliyopinda, hadi pale yatakaponyooka.

Hoja hii ninaikabidhi jumuiya ya wanablogu Tanzania, JUMUWATA, ikifaa ifanyiwe kazi na isipofaa itupiliwe mbali.

Naomba kuwasilisha!

Thursday, September 27, 2007

WABADILIKE WATUTUMIKIE AU WAJIUZULU WAKALIME

Wakati tuliousubiri haukuwa mbali sana kama nilivyofikiri, wakati huo si tu kuwa umekaribia bali umefika.

Kila kilichofichwa kichakani kitawekwa juu milimani na kila kilichofichwa gizani kitawekwa kweupe nuruni, ili kila mwenye macho aone.Bonyeza hapa uone yale yaliyofichwa ambayo Dk Slaa ameyafichua, tunamshukuru Mwanakijiji kwa kutuwekea ripoti hii ya Dk Slaa.

Hatuwezi kuufumbia macho ubadhirifu unaotendwa na viongozi wetu,hawa mafisadi wanaoutenda na wajue sasa kwamba siku zao zinahesabika, kwa kuwa viongozi wao waliowateuwa wanawahifadhi na kuwaonea aibu kuwawajibisha sasa wananchi wanawaanika kweupe, wachague sasa kujiuzulu na kwenda kulima au kubadilika na kuwatumikia wanachi kwa uaminifu.

Wasidhani tumelala tunawaangalia kwa macho mawili.

KISWAHILI NA KIINGEREZA KIPI ZAIDI?

Bila shaka usomapo unajibu la swali hapo juu?, najiuliza tu.Waafrika tuna kaugonjwa fulani kakudharau cha kwetu. Ndio.Yawezekana ni athari za ukoloni, waliviita vya kwetu vya kishenzi nasi tukaviona hivyo na kuvitukuza vya kwao na hii iko hadi leo.
Hii imepelekea kuiga kila cha mzungu, angalia leo utamaduni wetu ulivyopindapinda, haueleweki,sijui ni nini utambulisho wa mtanzania wa leo.Mimi nadhani ni Kiswahili chake tu!

Angalia dada zetu vivazi vyao, kuna wakati kulikuwa na uvumi kuwa presidenti wetu kapiga marufuku aina fulani ya vivazi vya dada zetu,wao wanaita vya kizungu,wengine waita vya kihuni!, jamaa wakazua kuwa mgambo watatanda na bakora halafu aonekane binti na kivazi cha kutatiza,analamba viboko kadhaa kama adhabu na onyo.Siku moja waandishi wa habari wakapata upenyo wakamuuliza mkuu, akajibu hana mpango wa kuchukua hatua hiyo, hayo ni mambo ya fashion tu, yatapita kama zilivyopita suruali za chini nimwagie miaka ileeeeeeeee. Vijana wa kiume wa kileo nao wamekuwa wazungu, wanasuka nywele, suruali zinavaliwa chini ya matako, ati mambo ya kizungu!.Mambo ya kuiga hayo!
Ni kwa vipi tutaweza kuulinda utamaduni wetu ulioingiliwa na utandawazi?

Leo hii tunaona kiingereza ni bora kuliko Kiswahili, tunaona hakifai kutumika kama lugha ya kufundishia, kama lugha inayofaa kutumika maofisini.Je tatizo hili ni la lugha au wenye lugha?.Si kuwa lugha ya kiswahili haiwezi kubeba kazi hizi, wenye lugha wameidharau lugha yao wamekitukuza kiingereza zaidi.Yawezekana kuwa lugha hii ina mapungufu lakini upungufu huu hauhalalishi kutokufaa kwa lugha hii, upungufu huu ni changamoto kwa wataalamu wetu wa kiswahili waweze kukiwezesha kiswahili kujitosheleza kutumika, mitaani kuwasiliana, mashuleni kufundishia, maofisini kwa mawasiliano ya kikazi.Wataalamu wetu watafsiri kwa kiswahili fasaha kila kilicho kwa kiingereza kiandikwe kwa kiswahili, kila kitu, vitabu vya mashuleni,maofisini,sheria zitumikazo mahakamani, vitabu vya maelekezo kwa wakulima juu ya matumizi ya mbolea na umwagiliaji,mikataba yote nchi hii inayoingia itafsiriwe pia ili wale wasio ijua lugha ya kiingereza waelewe yaliyoandikwa.

Kuna mwalimu wangu mmoja alinifundisha hesabu, tuition, enzi hizoooooooooooo, alijulikana kwa jina la ‘Mr So Much’, anasagia kwelikweli kiswahili anasema hakifai, anatupa mfano, anasema, kama kiswahili kingetumika kufundishia ingekuwa taaaabu kwelikweli, anatoa mfano, hapo anafundisha topic ya calculus, differentiation, sentensi kama ‘we differentiate y with respect to x’,dy/dx, tungesema ‘tunanyambulisha x kwa heshima ya y’, hapo hoja yake inakuwa kiswahili hakitoshi kufundishia na anatushawishi.Kwa wakati ule alitushawishi wengi tukakubali kuwa kiswahili hakifai kufundishia.Nadhani kina mapungufu yanayohitaji kurekebishwa na kuboreshwa.

Ukweli ulio wazi ni kwamba kiingereza ni kikwazo kikubwa kwa wanafunzi kuelewa masomo yao darasani na kufaulu usahili wanapoomba ajira.Endapo Kiswahili kitatumika kama lugha ya kufundishia kitamuwezesha mwanafunzi kuyapokea maarifa anayopewa na mwalimu wake kwa urahisi zaidi, ilivyo sasa mwanafunzi inabidi amsikilize mwalimu, atafsiri kinachofundishwa kutoka kiingereza kwenda kiswahili,akifanyie kazi akilini na kukihifadhi kwenye ubongo.Akishindwa kutafsiri alichosikia atashindwa kuelewa pia, hata kama atakiweka kwenye ubongo atakuwa amekariri tu na hili ndio tatizo tulilonalo hapa Tanzania.Ndio maana elimu yetu ni bora lakini haitoi maarifa ya kutosha kutuwezesha kupiga hatua mbele kiuchumi,kiteknolojia na kijamii.

Kama kiingereza kinaweza, kiswahili pia kinaweza, ingawa safari ya kukiwezesha ni ndefu na si rahisi!

Monday, September 17, 2007

Dk SLAA NI MFANO WA KUIGWA AUNGWE MKONO NA WATANZANIA WOTE!

Jana nilikuwa na usongo kweli wa kujua siku ya jumamosi ni watu gani ambao Dr Slaa aliwataja kama alivyoahidi,yaani wale wanaohusika na ubadhirifu wa fedha ya umma, kama ilivyo ada kwangu kwa siku za jumapili ninaelekea kanisani, kichwani nimepanga nikitoka tu nilisake gazeti lenye majina hayo. Nashawishika kununua gazeti la mwananchi lenye kichwa cha habari "Dk Slaa ataja vigogo wanaoitafuna nchi".Nilidhani ntayakuta majina mle ndani niwajue mafisadi hawa, wadau wa umasikini wa mtanzania azungukwaye na utajiri wa kila aina.

Kwa mshangao mkubwa sioni jina hata moja, zaidi ya kuona hawa waandishi wetu wa habari wanaandika,"miongoni mwa waliotajwa na Dk Slaa ni makatibu wakuu, wabunge wawili na mawaziri".Yaani kiujumla tu namna hiyo, halafu ndo imetoka.Hivi waliogopa nini kusema majina, mimi sijui taratibu za waandishi kwani hiyo si taaluma yangu, lakini wao si wangemnukuu tu Dk Slaa alichosema, tangu lini mjumbe akauwawa?

Kama na wewe hukuridhishwa na habari za vyombo vyetu vya habari siku ile basi tupia jicho pale kwa Mzee Mwanakijiji, amerusha hotuba ile msikilize na umsome kwa kubonyeza hapa.

Waandishi wa habari ni wakati sasa muanze kuthubutu kuwataja watu kwa majina jamii iwajue, hawa mafisadi ndio maadui wa uchumi wetu, hawa ndio maadui walioongezea wale kina ujinga, maradhi na umasikini, yaani amaadui hawa wametutengenezea adui aitwaye ufisadi au rushwa.Hawa wanapaswa kuchunguzwa na ikithibitika tuhuma zinazowakabili ni za kweli wafilisiwe na waukabili mkono wa sheria.

Hatuwezi kupiga hatua mbele kiuchumi kama tutaendelea kuwakumbatia hawa wezi, mafisadi wanaoitafuna nchi yetu,huku ndugu zetu wakikosa huduma bora za afya, elimu, maji safi, makazi bora nk

Tunataka kuona kuwa ile kauli mbiu ya maisha bora kwa kila mtanzania haikuwa danganya toto ya kupatia kula 'kura' bali ilikuwa na nia ya kweli ya kuboresha maisha ya mtanzania.

Takukuru nao wazifanyie kazi taarifa hizo, wawachunguize, kwani ni kazi yao.

Kitendo alichokifanya Dk Slaa ni cha kijasiri na cha kuungwa mkono na watanzania wote.

Tuamke sasa tupambane na maadui wa uchumi wetu.

Tuesday, September 11, 2007

SEPTEMBER 11

Tarehe hii ya leo mawka 2001 itabaki kuwa ya kukumbukwa, ni siku ambayo dunia ilishuhudia unyama na ukatili wa hali ya juu.Ni tukio la kigaidi lililoitikisa dunia. Angalia picha hii ujionee tukio hili la kikatili na kwa habari zaidi angalia hapa.

Friday, September 7, 2007

KILA LA KHERI TAIFA STARS


Kesho wawakilishi wetu, Taifa Stars wanachuana na Msumbiji ndani ya uwanja mpya.

Tuna njaa, kiu na shauku ya ushindi, tunataka kuiona timu yetu ikitoka uwanjani na ushindi na tuna kila sababu ya kushinda katika uwanja wetu wa nyumbani.

Taifa Stars oyeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeeee!

Mungu ibariki Taifa Stars!

Mungu ibariki Tanzania!

Sunday, August 19, 2007

MKATABA WA MADINI WA BUZWAGI ULISAINIWA CHURCHIL HOTEL UINGEREZA!

Mvua kubwa inanyesha, watu hawabanduki,mi nimejibanza kwenye mwamvuli wa jamaa nimekutana naye pale, kanihifadhi, ikitulia wanaume wanavua mashati wanakamua maji wanayavaa mashati yao tena, wana usongo kweli kweli wana hamu ya kumpongeza na kumsikiliza mbunge Zitto Kabwe ambaye hivi karibuni wabunge wa CCM wamememhukumu kwa kulidanganya bunge na hivyo kupewa adhabu ya kumzuia kuhudhuria vikao vya bunge hadi januari mwakani.

Mbunge Zitto kakaribishwa kuzungumza, kutokana na mvua iliyokuwa inanyesha waongeaji waliomtangulia walikuwa wakitumia mwamvuli, Zitto alivyoingia, akauliza,”kuna umuhimu wa kutumia mwamvuli?”, akaomba waondoe mwamvuli, akahutubia huku mvua inamnyeshea sawa na wale wanaomsikiliza.

Zitto kaongea mambo mengi makubwa yanayoonyesha uozo ndani ya mfumo uliopo unaokwamisha rasilimali zetu kulinufaisha taifa.

Kabla hajaanza kuhutubia, anawaomba wananchi wasimame na kuimba wimbo wa Tanzania Tanzanai. Nakupenda kwa moyo wote …………………………

Kuonyesha dhamira ya kuujenga upya uzalendo wetu uliopotea na wasio nao wabunge wetu wa chama tawala kwa kutanguliza maslahi ya matumbo yao na chama chao.

Anatuambia mwalimu wangu nje ya darasani, prof Issa Shivji aliniambia” Doubt everything” akiwa na maana “tilia shaka kila kitu”.Baada ya kutilia mashaka mkataba wa Buzwagi ndio maana akaamua kwa kushirikiana na wabunge wenzake wa upinzani kuwasilisha hoja binafsi ya kuundwa kwa kamati teule ya bunge kuchunguza mapitio ya mikataba ya madini na mazingira ya kusainiwa mkataba mpya wa madini wa Buzwagi.

Akiongelea mkataba uliosainiwa anasema, namnukuu,”Mkataba ulisainiwa Churchil Hotel London, kwa kuwa mkataba huu ulisainiwa Uingereza ulipaswa kusainiwa kwenye ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza, ubalozi wa nchi ni nchi”.

Hili la mkataba kusainiwa hotelini linashangaza, na lilituacha wasikilizaji midomo wazi!

Waziri Karamagi alipaswa kutueleza ilikuwaje, na bado anapaswa kutueleza ilikuwaje akaacha kwenda kwenye ubalozi wetu kuifanya kazi hii akaenda hotelini?

Cha ajabu tumeambiwa, mkataba wa Buzwagi umesainiwa rais akiwa hajui,hapa napo sielewi!

Serikali ilisimamisha kusainiwa mikataba mipya hadi mikataba ya zamani ipitiwe upya ili iweze kulinufaisha taifa, hili alilisema rais mwenyewe.

Swali lilozuka ni kwamba ni kwa nini mkataba huu usainiwe tena kwa vigezo vya zamani ambavyo vina mapungufu mengi, yanayopfanya tusinufaike na madini yetu.Hapa kuna maswalia mbayo waziri Karamagia anapaswa atujibu kiufasaha.

Bila shaka CCM hawakujua kuwa kwa kumtimua Zitto wanajitafutia ubaya na umma wa watanzania!, bila shaka sasa wanajuta!.

Ni watu kama Zitto ndio watakaoleta mabadikliko.

Aina ya watu watetezi na wapambanaji kama Zitto ndio wananchi wa nchi hii wanaowahitaji!

Kwa yoyote aliyekuwepo kwenye mkutano ule jambo moja lilikuwa wazi ni kwamba wananchi wamechoka, hawaoni wanaozipigania haki zao na kuwatetea ndani ya serikali iliyopo, hakuna mapambano ya dhati dhidi ya ufisadi.Sasa wanataka mabadiliko. Watu kama Zitto ndio wanaonekana wakombozi.

Sasa tunaikumbusha serikali hii yale yaliyosemwa katika Azimio la Arusha,

“Tumeonewa kiasi kutosha,tumenyonywa kiasi cha kutosha, tumepuuzwa kiasi cha kutosha. Ni unyonge wetu ambao umefanya tuonewe, tunyonywe na tupuuzwe.Sasa tunataka mapinduzi kuondoa unyonge wetu, ili tusinyonywe tena,tusionewe tena na tusinyanyaswe tena”.

Haiwezekani na hatukubali kuendelea kuwa taifa la waoga, mazuzu na mandondocha, kwani woga wetu ndio mtaji wa mafisadi . Mafisadi hawa husema, “watanzania wanasema mchana, usiku wanalala wakaimka wameshasahau”,sasa tunawajulisha tu kuwa, siku zao zinahesabiwa, waache ufisadi tulijenge taifa letu.Wabunge wa CCM mpo hapo?

Hembu watanzania tulivae koti la ujasiri na tupambane na mafisadi.

Nanukuu kama alivyosema Mrema leo” Heri kuishi kama Simba siku moja kuliko kuishi kama inzi siku mia moja”

Dk Slaa “Mwizi ntakufa nae”

Free Mbowe “ Haki haiombwi , hudaiwa”

Serikali yetu na isome alama za nyakati, ichukue hatua dhidi ya mafisadi.

Mkutno wa leo umefungua ukurasa mpya wa mapambano dhidi ya ufisadi. Mapambano haya hayana budi kuendelezwa na wananchi wote, wabunge wote, pamoja na wale wa CCM na viongozi wote.

Palipo na mafisadi hakuna maendeleo.

Penye nia pana njia.

Mungu ibariki Tanzania

Mungu tuepushea na mafisadi

Thursday, August 16, 2007

ZITTO KABWE ASIMAMISHWA UBUNGE!

Kama kuna mbunge ambaye anastahili ‘tuzo’ kwa kuiitenda kazi yake ipasavyo, nionavyo mimi mbunge huyo alipaswa kuwa ni Zitto Kabwe. Zitto ameonyesha kuwa shujaa na mwanamapinduzi anayetazamia kuiona Tanzania mpya kwa kujaribu kuitumia nafasi yake ya ubunge kuuondoa uozo ndani ya utawala uliopo!

Hapa ndipo ninapotamani kuanzishwa kwa tuzo hii, yawezekana isiwe ni pesa, kama ile zawadi inayotolewa na mfanya biashara maarufu, mwana wa Afrika,raia wa Sudan, Mo Ibrahim, ambaye amehaidi kuitoa kwa kiongozi atakaye kuwa muadilifu barani Afrika.

Tunaweza kufanya hivyo kwa wabunge watumishi wa watu, kama Zitto Kabwe ili kuwapa moyo kuendelea kupambana na mafisadi.Tuzo hii iwe ni ishara tu ya kuuthamini mchango wa mbunge husika ili ajue usahihi wa hoja anazozisimamia na nguvu ya umma iliyo nyuma yake.Nguvu ya mwanasiasa yoyote ni watu.

Iko wapi haki?,

Iko wapi demokrasi?,

Yako wapi maslahi ya taifa wanayoyalinda wabunge wetu?, mbona wamemtosa mpiganaji hodari aliyehitajika sana nasi wenye nchi?

Mbona Zitto kahukumiwa kukaa nje ya bunge hadi januari mwakani huku akiwa analitetea taifa lake linufaike na madini yake?

Je kuna tatizo gani kuchunguza mkataba uliosainiwa na waziri Karamagi katika mazingira ya utata tena ukasiniwa huko London na si hapa Tanzania?

Hili ni bunge la aina yake!

Yaani pale ndani we unga mkono tu!

Gongo gonga yale ma meza mara waziri akiwa anaongea kuashiria unakubaliana naye!

Kuna wakati Freeman Mbowe alilifananisha bunge letu na mchezo wa kuigiza!, mbunge wa chama kinachotawala hata kama amepinga hoja kwa manneno yake akimaliza kuongea anaiunga mkono kwa asilimia mia!

Swala aliloibua Zitto lilikuwa ni la msingi, wabunge wetu hawakuuona umsingi wake, wameangalia maslahi ya chama chao na matumbo yao na wakamtosa shujaa na mtetezi wetu ili kulinda maslahi yao na chama chao!

Hii ndio Tanzania yetu!

Hatuna budi kuipanga upya!

Hapa ilipo ni shaghalabagala!

Natamani Mwalimu Nyerere angalikuwa hai ayaone haya yanayotendeka ndani ya ardhi ya taifa aliloliasisi, najua asingalijizuia kuyakemea, potelea mbali hata kama wasingalimsikia. Kwa kuwa Mwalimu hayupo na tuwaambie hawa wabunge wa CCM mwendo huu wa kuwanyamazisha mashujaa na watetezi wetu siyo wenyewe!

Wapo wanaharakati walioanza kulisema hili.

Kuendelea na kautaratibu ka hovyo kama haka ka kuwasimamisha ubunge wabunge wenye hoja za msingi, kwa kisingizio chochote kile, ni kujenga bunge la wabunge waoga na kuendeleza taifa la mazuzu.

Ni kutowatendea haki watanzania.

Aluta kontinua!

Friday, August 10, 2007

ITAKUWAJE 2025?

Jiji la Dar es salaam linakuwa kwa kasi.

Cha ajabu ni kwamba mambo mengi yamebaki vile vile, yanayooongezeka hayaoani na idadi ya wakazi weanaozidi kuongezeka jijini kila kukicha. Kasi ya kuleta maendeleo yanayokidhi idadi ya watu ni ya mwendo wa konokono.

Bila kuendeleza vijiji, kupeleka huduma bora za kijamii kama elimu,afya,mabenki,umeme,watu wataendelea kukimbilia mijini!

Jiji limejaa,najiuliza ni lini wakuu wetu watahamia Dodoma kule wanakotuambia ndio mji mkuu wa nchi yetu, kila mmoja anataka kukaa Dar, viongozi nao hawataki kuhamia Dodoma.Wasomi wetu nao wanajazana Dar.Kuna nini Dar kisichowezekana kwingine?,Nani atakeayepeleka maendeleo hizo sehemu nyingine ikiwa kila mmoja asema “tutabanana hapa hapa”?, wabunge nao wakaa jijini, majimboni kwao wanakaa lini?,kaaazi kweli kweli!

Labda kuhama kwa wakuu na idara zao kutapunguza msongamano barabarani.

Asubuhi na jioni usafiri ni vurugu tupu. Wakuu hawaelewi taabu hii inayompata binadamu, raia na mkazi wa jiji hili Dar es salaam.Kama wanaelewa haliwakeri.Angalia watu wanavyopanda kwenye mabasi kupitia madirishani,angalia taabu anayoipata mwanafunzi ndani ya jiji hili.

Ndio maana natamani ndugu Lowasa akakae Mbagala japo kwa wiki moja, apande daladala kama sisi, aone taabu ya usafiri inavyomlazimisha kijana mtanashati kuuacha mlango na kuingilia dirishani, mradi tu aweze kuwahi kazini. Juzi kijana mmoja amefariki, akiwa anagombea daladala akaanguka ,gari ikamkanyaga,mauti ikamfika.

Ndio maana natamani ndugu Kandoro akakae Kigamboni japo kwa wiki moja tu aione taabu inayomkabili mtanzania anayetumia kivuko kibovu pasipo uhakika wa usalama wa maisha yake.

Ndio maana natamani mama Magret Sitta ahamie Gongo la Mboto japo kwa wiki moja ili aone jinsi wanafunzi wanavyopata taabu kupata usafiri wa kwenda na kurudi shuleni.

Jiji limejaa, endapo hali ikiendelea hivi ilivyo, je 2025 itakuwaje?, patakuwa hapatoshi!

Tutafakari!

Sunday, July 29, 2007

TUNAHITAJI MABADILIKO

Mabadiliko ya kweli hutoka chini kwenda juu,binadamu ni mwepesi wa kusahau alikotoka,pale anaposhiba humsahau mwenye njaa, ndivyo ilivyo kwa viongozi wetu hawaguswi na matatizo yetu raia tuliowachagua, watarudi kwetu kuomba kura 2010. Ndani ya Serikali wanalindana,hakuna anayewajibishwa, ndani ya bunge wanatetea maslahi ya chama badala ya maslahi ya taifa na watu wake. Ndani ya mahakama nako kunanuka rushwa, pale ambapo tunategemea kuipata haki, sheria hulegezwa na pesa!. Ukikwama unaambiwa nyoosha mkono mambo yatakaa sawa.Kwa mwendo huu hatufiki kokote. Ni lazima tubadilike. Mambo haya mengi yaliyooza ndani ya mihimili yote mitatu ni matokeo ya mfumo mbovu, ndio maana iko haja ya kuwa na mjadala wa kitaifa wa kuyaangalia mambo haya kwa undani, ndiyo maana iko haja ya kuibadili katiba yetu tuupange sawa mfumo mzima wa mihimili ya dola.Kutokufanya hivi ni kuuendeleza uozo kwa vizazi vijavyo.Kama tunasema Serikali hii ni ya watu iliyowekwa na watu kwa ajili ya watu ni kwa nini ione kigugumizi cha kutunga katiba mpya.Bila kumung'unya maneno, katiba iliyopo sasa haifai, no checks and balance!

Iweje leo watu waliotukosea kama taifa kwa kusaini mikataba mibovu huku wakila ten percent waendelee kukalia ofisi zao?,Mwalimu aliwainisha maadui watatu wa maendeleo yaani ujinga, umasikini na maradhi sasa tuuongeze na ufisadi. Kiongozi asiyeweza kupambana na ufisadi hafai tumkatae.Wamesaini mikataba ya Richmond,ATCL,IPTL na mingine.Je hawa si wezi wanaotakiwa kushughulikiwa?Mimi hujiuliza nini maana ya kumchoma moto mwizi anayeiba kuku mtaani na kumuacha huyu fisadi na mwizi anayetuibia mabilioni?,siungi mkono kuchoma wezi moto, ninachohoji ni kwa nini hatuoni ulazima wa kuwataka hawa wala rushwa wapishe viti
na kuukabili mkono wa sheria?

Raisi Kikwete aliwahi kutueleza kuwa anawajua wala rushwa kwa majina akawapa muda wajirekebishe.Kwa kuwa hawajajirekebisha, anangoja nini kuwatimua?, Hii ni alama gani kwa utawala wake?

Wauza dawa za kulevya majina yao tuliambiwa yamekabidhiwa kwa vyombo vinavyohusika.Hadi leo kimya! Mimi sielewi. Huu ni uozo mwingine.Nani anayepiga kelele tena juu ya biashara hii chafu baada ya sauti ya shujaa Amina Chifupa kunyamazishwa na kifo?, nitajieni jina la mbunge mmoja tu aliyeanza kumuenzi Amina kwa kuendeleza mapambano dhidi ya madawa ya kulevya.Haya madawa yanateketeza vijana wetu, Amina alilitambua hili akalishikia bango, sasa Amina hayupo, ni nani anayesema aluta kontinua?

Leo hii kuna vijana wa Tanzania wapatao 24 ambao Serikali imewakana kule Ukraine.Imesema walienda kwa njia zao wenyewe na serikali haiopo tayari kuwapa mkopo waendelee na masoma yao.Mimi najiuliza hivi hata kama wamekosea si wangeelezwa tu waombe radhi kwa barua kukiri kosa na kuendelea na masomo yao?Hivi kosa lao la sasa si ni faida ya taifa kwa baadae?Au wasomi tulionao leo wanatosha?Je ni nani asiyejua kuwa elimu ya nchi za nje huko ughaibuni ni bora kuliko ya kwetu hasa kwa kuwa wao wameendelea kisayansi na kiteknolojia kuliko sisi? Serikali isiniambie kuwa haina hela, ninajua kuwa zipo na zinatumika vibaya bila ya kuwajibishana achilia mbali magari ya kifahari wanayotembelea viongozi wetu. Hembu wanieleze waliotumia vibaya fedha ya serikali kama ilivyoonyeshwa katika ripoti ya Chief Auditor General wamefanywa nini?,hii hela iliyopotea ingeweza kuwalipia hawa vijana kule Ukraine na chenji ikabaki ya kuwalipia na wengine.Huu nao ni uozo mwingine.Wabunge wetu wameshindwa kuwatetea kwa kuwa wanawakilisha chama bungeni, wale wa upinzani walijaribu kwa nguvu zote kuwatetea lakini sauti zao bado ni ndogo kwa kuwa idadi yao ni dogo, ujumbe tunaoupata sisi raia ni kwamba tuiogeze idadi ya wabunge wa kambi ya upinzani bungeni wakatutetee.Pamoja na wabunge kushindwa umma wa watanzania nao umeshindwa kuwaokoa wale vijana japo hata kwa maandamano ya amani, hapo ndipo viongozi wetu wanaona watanzania ni watu poa sana, hawana noma kabisa. Bila shaka raia wa nchi hii ni wapole kuliko raia wote duniani, upole wa kusikia kukubali na kutopinga jambo lolote hata kama lina madhara kwetu. Tusipobadilika majirani zetu , Kenya na Uganda wataendelea kutudharau.Eti tuna amani na utulivu!, mimi si ukubali upuuzi huu,kilichopo ni woga na uzuzu!

Tutakuwa na amani na utulivu tutakapokuwa na Serikali inayosikiliza shida za watu na kuzitatua, inayopambana na wala rushwa wakubwa na wadogo, inayowajali masikini,inayowawajibisha watumishi wake wanapokosea,inayotoa haki kwa wote bila kujali nguvu ya pesa,inayotumia mali asili yake kwa manufaa ya raia wake,inayotoa elimu bora kwa watu wake.
Tunakuwaje na amani na utulivu wakati tunaibiwa na viongozi mabilioni kwa kutia saini mikataba yenye utata?, mimi sielewi!

Bunge nalo sijui kwa nini limegeuka kituko, ni bunge la aina yake duniani!. Ukweli huwa mbaya ukiangaliwa vibaya.Nikisema kituko sitanii. Hembu fikiria mbunge anaongea anpinga zaidi ya asilimia sabini na tano ya hoja fulani ya Serikali au bajeti ya wizara fulani halafu mwishoni anasema "mheshimiwa spika naunga mkono hoja".Mimi sielewi.Naona usanii mtupu.Ile speed and standard imegota sawa tu na ile ari, nguvu na kasi ambayo tuliambiwa kuwa sasa zingekuwa mpya.

Ni mara mbili nimewasikia wabunge wakimpongeza raisi Kikwete,si vibaya kumpongeza.

Mara ya kwanza walimpongeza kwa kuiilaani filamu iliyotengenezwa na Hubert Sauper ya Darwin’s Nightmare ijulikanayo kama Filamu ya mapanki kwa kuwa imeidhalilisha nchi yetu.Hoja hii iliwasilishwa na mbunge Mudhihir Mudhihir iliungwa mkono ikachangiwa kwa kishindo!
Kwa kuwa raisi alisema atashugulukia mikataba sasa wamuunge mkono kwa hili pia, wawasilishe hoja ya kuwalaani wale wote walioiigiza nchi yetu kwenye mikataba mibovu na wala rushwa wote.Hawa ndio maadui wa maendeleo yetu.

Mbunge wa Ukerewe Getrude Mongela akawasilisha hoja, eti anampongeza raisi kwa kuwaita watendaji wa serikali na kujadili ripoti ya Chief Auditor General.Ripoti ilionyesha wajanja wamekula hela.Wamempongeza raisi kwa lipi?, si alikuwa anatimiza wajibu wake?Je ni wezi wangapi katika hao waliohusika kama ilivyoonyeshwa ndani ya ripoti hiyo wamechukuliwa hatua?,ningeiona mantiki ya kumpongeza kama angewafukuza kazi wote walioiba fedha ya serikali.

Wabunge hawa wameiacha bajeti inayomkandmiza mtu duni ipite, siku ya kwanza ya machungu ya bajeti hii ni pale nauli zilipopanda, za mikoani kisha za daladala jijini Dar es salaam.

Naongea na kijana mmoja ndani ya daladala tarehe 25 July 2007 siku ya kwanza nauli ya daladala kupanda jijini Dar es salaam:

Ananiambia "Sijui itakuwaje maisha yanapanda mishahara iko pale pale, kwa nini wasiangalie
sekta binafsi, mishahara yetu midogo sana"

Namuuliza "Kwani unatokea wapi?"

Anajibu " Magomeni napanda hadi Drivin kisha natembea hadi macho pale CCBRT ,ni mwendo
wa kama dakika kumi hivi, halafu napanda gari la Masaki"

Namuulza "Kwani unalipwa shilingi ngapi?"

Anajibu " Ni elfu arobaini na nae, miezi mingine wanatoa nauli inaongezeka inafika elfu 60"

Jamaa anatumia elfu thalathini na tatu kwa mwezi nauli tu,anabakiwa na elfu kumi na tano!, Ni sauti gani ya utetezi inayotoka kwa mbunge anayemuwakilisha kijana huyu?Haya ndio mambo ya kupigia kelele bungeni, hadi kieleweke!, ukweli ni kwamba wafanyakazi wengi wananyonywa, hapa ninaongelea sekta binafsi.Hivyo unyonyaji bado ungalipo.Nani anawatetea hawa bungeni?

Umefika wakati sasa raisi Kikwete afahamu kuwa tunataka kuiona nchi inasonga mbele. Kwa sasa imegota.

Umefika wakati wabunge wetu wafahamu kuwa hatukuwatuma kuwakilisha chama na kulinda maslahi ya chama chao.Tumewatuma kulinda maslahi yetu na taifa letu, wakishindwa hawastahili kuendelea na kazi. Wasidhani tumelala,tuko macho tunawaangalia wanavyoitenda kazi tuliyowatuma, ambayo kwa sasa utendaji wao ni duni mno.

Wateteeni watu wetu.

Ondoeni unyonge wa watu wetu dhidi ya waonezi wetu.

Pambaneni na ufisadi unaowazunguka watu wetu.

Huu ni wajibu wenu, muutimize.

Tunahitaji mabadiliko.

Monday, July 9, 2007

Kauli ya Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa,Ban Ki-Moon

“Mazoea yangu kila siku asubuhi huenda hayatofautiani na yako. Tunachukua magazeti na kufungua television,iwe mjini New York,Lagos au Jakarta kuangalia mateso ya kila siku yanayomkabili binadamu.Inawezekana kuwaDarfur,Lebanon au Somalia”

Anaendelea …………………………. na kumalizia,

“Kila asubuhi tunaweza kusoma kwenye magazeti. Lakini ni kwa jinsi gani tunasikiliza sauti za watu hao au kujaribu kwa nguvu zote na kwa kudhamiria kuwasaidia?Nawaomba mfanye hivyo”

Hii ni kauli nzito inayotoka kwenye hisia kali za kiongozi anayewajali watu anayewaelekeza viongozi kuwa watumishi wa watu.Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Ban Ki-Moon anachojaribu kuwaeleza viongozi hawa ni kuwa haya mateso tunayoyaona kwenye runinga, tunayoyasoma kwenye magazeti na tunayoyasikia kwenye radio wasiyapuuze, wasiyaangalie tu, wasiyasome tu.Wayatatue kwa nguvu zao zote.

Ni kama vile anawaambia huu ni wajibu wenu muutekeleze.

Ni kama vile anawaambia mshikwe na huruma mnapoona na kusoma matatizo yanayowazunguka watu wenu na kuutafuta ufumbuzi wa matatizo hayo.

Ni kama vile anawaambia msiidharau sauti ya watu inapobeba kero zao na kuzileta kwenu, zitatueni kero zao.

Ni viongozi wanagpi tulionao hapa Tanzania wanaolitekeleza ombi hilo la Katibu mkuu kwa vitendo?,Wananchi wengi ukiwsaikiliza wamechoka, wamepoteza matumaini kwa viongozi waliowachagua. Hakuna anayemjali mskini.Koti la umaskini wa watu wamelitupa, watalivaa tena wakati wauchaguzi ukiwadia. Ndio nchi hii ilipofikia.Watanganyika sasa wanaitwa Wadanganyika!.Tunadanganywa na viongozi miaka mitano mitano!

Hivi yale maisha bora kwa kila mtanzania tuliyoambiwa yako wapi?

Kwa mujibu wa nukuu ya Ban Ki-Moon hapo juu, ni kiongozi gani, ni mbunge gani anayeweza kunyoosha kidole akasimama akatueleza namna anavyotumia mudawake kutatua kero za watu anaowaongoza?. Unatoka wapi uhalali wa viongozi butu kama hawa kuendelea kuongoza?. Mbona hawazisikii sauti za watu na kuwasaidia?

Wa kale walisema “sauti ya watu ni sauti ya Mungu”,mbona wameikana busara hii ya wazee wetu wa zamani?

Kuna ufisadi mwingi unaotuzunguka, kuuacha upite nakuendelea kwenye kizazi kijacho ni kutokitendea haki kizazi hicho cha wana wetu na wana wa wana wetu.Ni kutokuwajibika.Iwe kwa mijadala au njia yoyote ile tunahitaji mabadiliko!Mbona tuliupigania uhuru, lakini matunda yake tumeyaacha yawafaidishe wajanja wachache?Hakika kizazi hiki kina jukumu kubwa la kufanya kuuondoa uozo uliopo.Mafisadi hawa wameingia mikataba mibovu kwa maslahi yao. Bado wengine wangali wakikalia viti vyao.Kwa nini?

Yule mkuu wa Benki ya dunia alipopata kashfa ya kumpandisha cheo mpenzi wake na kumuongezea mshahara,sasa amewekwa pembeni.Mbona hapa kwetu huyu mkuu wa benki kuu ana tuhuma za ulaji anaendelea kukalia kiti? Si inasemekana anatarajiwa kuchunguzwa?.Taifa hili linahitaji muelekeo mpya. Linahitaji kuwa na utaratibu wa kuwatambua wenye maadili wanaofaa kuongoza lakini pia kuwe na utarataratibu wa kuwachukulia hatua kali wanaokwenda kinyume na taratibu hizo bila kulindana.

Viongozi wetu watekeleze wito wa katibu mkuu, Ban Ki-Moon.

Mungu ibariki Tanzania,

Mungu ibariki Afrika.

Thursday, June 28, 2007

FRIJI ISIYOTUMIA UMEME

Hii ni habari njema.Habari hii nimeipata kutoka idhaa ya kiswahili BBC.Ni teknolojia itakayotuwezesha kutumia vyombo vya kupoozea kama vile friji bila ya kutumia umeme.Kilichonivutia zaidi, teknolojia hii ilikuwa ikiongelewa na mtanzania mwenzetu aliyefanya utafiti wake nchini Uingereza.Mwandishi wa habari wa BBC alipomuuliza mhandisi huyu,tarehe 13th March 2007, kuwa kwa nini akiwa kama mwafrika asiisaidie nchi yake kuileta teknolojia hii.

Anamjibu,

“Endapo viongozi wetu na watunga sera watataka kupata utaalamu wangu ili uinufaishe nchi yetu niko tayari”

Swali ninalojiuliza ni kwamba, ni kwa nini hawa tuliowapa dhmana ya kutuongoza hawana mikakati madhubuti na endelevu ya kuwatumia wataalamu wetu walioko ughaibuni hata waliopo nyumbani kwa manufa ya nchi yetu?

Je ni ubutu wa fikra?

Je ni kutokujua?

Au ni nini hasa?

Kuongoza ni kuonyesha njia. Kila mmoja atimize wajibu wake

Wednesday, June 27, 2007

BURIANI AMINA

Ni asubuhi, naamka na ninaingia mtaani katika pilikapilika zangu za kawaida, njiani naona gazeti lenye kichwa cha habari Amina hatunaye tena. Nashangaa!. Namuita muuza gazeti na kununua gazeti kupata undani wa kilichoandikwa.Baada ya kusoma nathibitisha kuwa Amina Chifupa ameaga dunia. Hatunaye tena.

Kweli chema hakidumu!

Mithili ya Amina Chifupa ndani ya CCM sijamuona. Mfanao wa mpambanaji jasiri dhidi ya ufisadi miongoni mwa wa wabunge wa chama kinachotawala ukimuondoa Amina mwingine simjui.

Nikiwa nimepigwa butwaa, nachukua simu yangu ya mkononi, kufungua blogu ya ndugu Michuzi nakutana na habari inayoeleza kifo cha Amina Chifupa, ikieleza kuwa Amina amefariki usiku wa kuamkia jana saa tatu kasorobo katika hospitali ya jeshi Lugalo alikokuwa amelazwa.

Kweli duniani tu wapitaji. Mungu aipe nguvu familia ya hayati Amina Chifupa kustahimili katika kipindi hiki kigumu.

Ningeweza kuishia kutoa pole kwa familia,nikamaliza. Lakini kuna mengi ya kusema juu yake, kwa kuwa alikuwa akifanya kile ambacho watanzania tulipenda kumuona akiendelea kufanya. Kupambana na ufisadi unaotuzunguka. Tunakumbuka jinsi alivyokuwa mstari wa mbele katika vita dhidi ya madawa ya kulevya. Amina alithubutu kufanya yale ambayo wengi hawana ujasiri wa kuyafanya,kuiondoa hali ya hewa chafu inayotuzingira, alikataa kuiona harufu hiyo chafu kama hali ya kawaida.Alikemea, alihoji na alisimamama kwenye haki.Alikuwa mtetezi wa watu duni.Watu wa aina hii si wengi miongoni mwa viongozi wetu wa leo.Ni kweli kuwa ameacha pengo kubwa, ndani ya chama alichokuwapo, sijamuona wa kuliziba.

Binadamu tu wasafiri, maisha yetu duniani ni mafupi, na tuishi kwa kutende mema kwa jamii ituzungukayo, walio katika nafasi za uongozi na wawapende na kutenda haki kwa wale wanaowaongoza ili siku ya kuondoka itakapowadia matendo yetu mema yaendelee kuishi na jamii tuliyoiacha.

Wote tuseme mapambano yanaendelea.

Kwa heri mpendwa wetu

Sunday, June 24, 2007

Karibuni wote

Nawakaribisha katika blogu hii tuweze kendeleza harakati za kujikomboa dhidi ya maadui watuzungukao yaani ujinga, maradhi na umaskini pamoja na kila aina ya ufisadi unaoendelezwa na mafisadi ndani ya mfumo wa kifisadi.
Mapambano hayajaisha kwani ukoloni unaendelezwa kupitia mlango wa nyuma na unyonyaji bado ungalipo.Mtu duni anaendelea kuwa duni na mwenye nacho anaendelea kuwa nacho kwa kumnyonya mtu duni asiye na sauti.Bila usawa hakuna haki. Ni jukumu letu sote kuupigania usawa ndani ya jamii tuishiyo kwani binadamu wote ni sawa na wote tuna haki ya kuishi maisha bora.