Sunday, August 19, 2007

MKATABA WA MADINI WA BUZWAGI ULISAINIWA CHURCHIL HOTEL UINGEREZA!

Mvua kubwa inanyesha, watu hawabanduki,mi nimejibanza kwenye mwamvuli wa jamaa nimekutana naye pale, kanihifadhi, ikitulia wanaume wanavua mashati wanakamua maji wanayavaa mashati yao tena, wana usongo kweli kweli wana hamu ya kumpongeza na kumsikiliza mbunge Zitto Kabwe ambaye hivi karibuni wabunge wa CCM wamememhukumu kwa kulidanganya bunge na hivyo kupewa adhabu ya kumzuia kuhudhuria vikao vya bunge hadi januari mwakani.

Mbunge Zitto kakaribishwa kuzungumza, kutokana na mvua iliyokuwa inanyesha waongeaji waliomtangulia walikuwa wakitumia mwamvuli, Zitto alivyoingia, akauliza,”kuna umuhimu wa kutumia mwamvuli?”, akaomba waondoe mwamvuli, akahutubia huku mvua inamnyeshea sawa na wale wanaomsikiliza.

Zitto kaongea mambo mengi makubwa yanayoonyesha uozo ndani ya mfumo uliopo unaokwamisha rasilimali zetu kulinufaisha taifa.

Kabla hajaanza kuhutubia, anawaomba wananchi wasimame na kuimba wimbo wa Tanzania Tanzanai. Nakupenda kwa moyo wote …………………………

Kuonyesha dhamira ya kuujenga upya uzalendo wetu uliopotea na wasio nao wabunge wetu wa chama tawala kwa kutanguliza maslahi ya matumbo yao na chama chao.

Anatuambia mwalimu wangu nje ya darasani, prof Issa Shivji aliniambia” Doubt everything” akiwa na maana “tilia shaka kila kitu”.Baada ya kutilia mashaka mkataba wa Buzwagi ndio maana akaamua kwa kushirikiana na wabunge wenzake wa upinzani kuwasilisha hoja binafsi ya kuundwa kwa kamati teule ya bunge kuchunguza mapitio ya mikataba ya madini na mazingira ya kusainiwa mkataba mpya wa madini wa Buzwagi.

Akiongelea mkataba uliosainiwa anasema, namnukuu,”Mkataba ulisainiwa Churchil Hotel London, kwa kuwa mkataba huu ulisainiwa Uingereza ulipaswa kusainiwa kwenye ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza, ubalozi wa nchi ni nchi”.

Hili la mkataba kusainiwa hotelini linashangaza, na lilituacha wasikilizaji midomo wazi!

Waziri Karamagi alipaswa kutueleza ilikuwaje, na bado anapaswa kutueleza ilikuwaje akaacha kwenda kwenye ubalozi wetu kuifanya kazi hii akaenda hotelini?

Cha ajabu tumeambiwa, mkataba wa Buzwagi umesainiwa rais akiwa hajui,hapa napo sielewi!

Serikali ilisimamisha kusainiwa mikataba mipya hadi mikataba ya zamani ipitiwe upya ili iweze kulinufaisha taifa, hili alilisema rais mwenyewe.

Swali lilozuka ni kwamba ni kwa nini mkataba huu usainiwe tena kwa vigezo vya zamani ambavyo vina mapungufu mengi, yanayopfanya tusinufaike na madini yetu.Hapa kuna maswalia mbayo waziri Karamagia anapaswa atujibu kiufasaha.

Bila shaka CCM hawakujua kuwa kwa kumtimua Zitto wanajitafutia ubaya na umma wa watanzania!, bila shaka sasa wanajuta!.

Ni watu kama Zitto ndio watakaoleta mabadikliko.

Aina ya watu watetezi na wapambanaji kama Zitto ndio wananchi wa nchi hii wanaowahitaji!

Kwa yoyote aliyekuwepo kwenye mkutano ule jambo moja lilikuwa wazi ni kwamba wananchi wamechoka, hawaoni wanaozipigania haki zao na kuwatetea ndani ya serikali iliyopo, hakuna mapambano ya dhati dhidi ya ufisadi.Sasa wanataka mabadiliko. Watu kama Zitto ndio wanaonekana wakombozi.

Sasa tunaikumbusha serikali hii yale yaliyosemwa katika Azimio la Arusha,

“Tumeonewa kiasi kutosha,tumenyonywa kiasi cha kutosha, tumepuuzwa kiasi cha kutosha. Ni unyonge wetu ambao umefanya tuonewe, tunyonywe na tupuuzwe.Sasa tunataka mapinduzi kuondoa unyonge wetu, ili tusinyonywe tena,tusionewe tena na tusinyanyaswe tena”.

Haiwezekani na hatukubali kuendelea kuwa taifa la waoga, mazuzu na mandondocha, kwani woga wetu ndio mtaji wa mafisadi . Mafisadi hawa husema, “watanzania wanasema mchana, usiku wanalala wakaimka wameshasahau”,sasa tunawajulisha tu kuwa, siku zao zinahesabiwa, waache ufisadi tulijenge taifa letu.Wabunge wa CCM mpo hapo?

Hembu watanzania tulivae koti la ujasiri na tupambane na mafisadi.

Nanukuu kama alivyosema Mrema leo” Heri kuishi kama Simba siku moja kuliko kuishi kama inzi siku mia moja”

Dk Slaa “Mwizi ntakufa nae”

Free Mbowe “ Haki haiombwi , hudaiwa”

Serikali yetu na isome alama za nyakati, ichukue hatua dhidi ya mafisadi.

Mkutno wa leo umefungua ukurasa mpya wa mapambano dhidi ya ufisadi. Mapambano haya hayana budi kuendelezwa na wananchi wote, wabunge wote, pamoja na wale wa CCM na viongozi wote.

Palipo na mafisadi hakuna maendeleo.

Penye nia pana njia.

Mungu ibariki Tanzania

Mungu tuepushea na mafisadi

No comments: